Senegal: Kambi inayopinga mfumo yataka tu mazungumzo kuhusu tarehe ya uchaguzi wa rais
Kambi ya Bassirou Diomaye Faye, mgombea urais anayeponga mfumo wa utawala anayezuiliwa jela nchini Senegal, imeonya kwamba itakataa kujadili chochote kile na mkuu wa nchi anayemaliza muda wake isipokuwa tarehe ya uchaguzi, iliyoahirishwa kwa muda usiojulikana.
Imechapishwa:
Senegal, iliyotumbukia katika mzozo wa kisiasa, kwa mara nyingine inashikilia neno la Rais Macky Sall ambaye anatazamiwa kulihutubia taifa leo Alhamisi jioni na anaweza kusema mipango yake ni nini kwa ajili ya kuandaa uchaguzi wa rais, uliopangwa awali Februari 25.
Baada ya kuona Baraza la Katiba likbatilisa wiki iliyopita agizo lake la kuahirisha uchaguzi na kuomba kuandaa uchaguzi "haraka iwezekanavyo", Rais Sall alisema nia yake ni kutekeleza "bila kuchelewesha mashauriano muhimu" ya kufanyika kwa uchaguzi. Hakuna kilichovuja rasmi kutoka kwa mijadala ambayo amekuwa akifanya tangu wakati huo.
Muungano wa Diomaye Président umemshutumu Rais Sall kwa kujikokota, katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyochapishwa usiku wa Jumatano kuamkia Alhamisi baada ya tangazo kwamba mkuu wa nchi atalihutubia taifa siku ya Alhamisi jioni. "Hakuna uhalali wa ucheleweshaji huu kudumishwa katika ngazi ya juu ya taifa," amesema. Anabainisha kuwa uchaguzi lazima ufanyike kabla ya kumalizika rasmi kwa muhula wa Bw. Sall, tarehe 2 Aprili.
"Unaweza tu kushiriki katika mashauriano ambayo madhumuni yake mahususi ni kurekebisha bila kuchelewa tarehe ya uchaguzi wa urais," amesema. Kuhusu mazungumzo yanayoweza kupanuliwa kwa masuala mengine, "yanaweza tu kufanyika baada ya rais ajaye kuapishwa," ameongeza.
Pia ametoa wito wa kuachiliwa kwa wale wote wanaozuiliwa kutokana na maandamano yaliyoikumba Senegal tangu mwaka 2021. Bw. Faye, nambari mbili wa chama cha zamani cha PASTEF kilichofutwa, yeye mwenyewe yuko kizuizini tangu mwezi Aprili 2023, sawa na mkuu wa chama hicho Ousmane Sonko.