Senegal: Rais Sall bado anatafuta tarehe ya uchaguzi wa urais
Rais wa Senegal anaendelea na juhudi zake siku ya Jumanne kufikia makubaliano juu ya tarehe ya uchaguzi wa urais uliyoahirishwa kwa muda usiojulikana, huku mashirika ya kiraia yakijaribu kuhamasishana ili uchaguzi ufanyike katika wiki zijazo.
Imechapishwa:
Vuguvugu la Aar Sunu ("Tuhifadhi uchaguzi wetu") limetoa wito kwa raia kusalia nyumbani na kuitikia mgomo wa jumla wakati ambapo mashauriano yaliyozinduliwa siku moja kabla na Rais Macky Sall yalikuwa yakiendelea ili kuondokana na moja ya migogoro mikubwa zaidi iliyoshuhudiwa nchini kwa miongo kadhaa.
Wito huo umeonekana kupuuzwa katika eneo la kati la Plateau na karibu na soko lenye watu wengi la Colobane huko Dakar: shughuli mbalimbali kama usafiri wa umma, zimeendelea kama kawaida, huku umati wa watu ukionekana karibu na maduka na shughuli zingine zikiendelea.
Saer Dieng, mfanyabiashara mwenye umri wa miaka 37, amefungua biashara yake ya nguo. "Tunaishi siku baada ya siku, hatuwezi kumudu siku bila kufanya kazi, vinginevyo familia zetu hazitakula." Badara Dione, dereva wa teksi wa pikipiki mwenye umri wa miaka 40, "hakuwa na taarifa yoyote kuhusiana na mgomo huu". Hata kama haungi mkono kuahirishwa kwa uchaguzi wa urais, "mgomo hautufai".
Vuguvugu la Aar Sunu "linamtaka" rais kupanga uchaguzi kabla ya Aprili 2, mwisho rasmi wa muhula wake. Aar Sunu ni sehemu ya mrengo mpana wa kisiasa na raia ambao umeundwa tangu Rais Sall alipotangaza Februari 3 kuahirishwa kwa dakika ya mwisho uchaguzi wa urais.