Uchaguzi Israel : Netanyahu atangaza kuwa ameshinda
Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amesema chama chake cha Likud kimeshinda katika Uchaguzi wa wabunge uliofanyika Jumanne wiki hii.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kauli hii ya Netanyahu inakuja wakati huu matokeo ya awali yakionesha kuwa chama cha Netanyahu cha Likud na kile cha upinzani kinachoongozwa na Yitzhak Herzog, vinachuana kwa karibu na hadi sasa kila chama kimepata viti 27 kati ya 120 vinavyowaniwa.
Akizungumza na wafuasi wake jijini Tel Aviv, Netanyahu amesema chama cha Likud kimepata ushindi mkubwa na tayari ameshazungumza na viongozi wa vyama vingine vidogo vidogo ili kuunda serikali mpya.
Hata hivyo kiongozi wa upinzani Yitzhak Herzog amesema chochote kinaweza kutokea na ni mapema mno kwa Netanyahu kuanza kusheherekea.
Herzog naye amewaambia wafausi wake kuwa ana uhakika wa kuunda serikali na kubadilisha uongozi wa nchi hiyo.
Huu ni mshangao katika uchaguzi uliofanyika Jumanne Machi 17 nchini Israeli. Orodha ya Waisraeli wenye asili ya Kiarabu imekua nguvu ya tatu katika Bunge la Israeli (Knesset). Muungano wa vyama mbalimbali vya Warabu, kulingana na matokeo ya mwanzo, ambayo yanatazamiwa kuthibitishwa Jumatano asubuhi wiki hii, umepata viti 13. Matokeo ambayo yameanza kusheherekewa katika mji wa Nazareti, mji mkubwa unaokaliwa na waarabu wengi nchini Israeli.
Matokeo ya mwisho yanatarajiwa kufahamika saa chache zijazo, na rais Reuven Rivlin atatoa nafasi kwa yule atakayeonekana kuwa na viti vingi ili kuunda serikali.
Ikiwa Netanyahu atafanikiwa kuunda serikali, atakuwa Waziri Mkuu wa Israeli aliyehudumu kwa muda mrefu wa mihula minne.