CAR : Seleka na Antibalaka wakubaliana kusitisha mapigano
Mkutano ambao umekua ukifanyika katika mji mkuu wa Congo, Brazzaville kuhusu namna ya kurejesha hali ya utulivu na amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati umemalizika jumatano wiki hii katika hali ya kutatanisha, baada ya makundi hasimu ya Seleka na Antibalaka kuweka saini kwenye mkataba wa kusitisha mapigano.
Imechapishwa:
Mapigano hayo yaliyochochea machafuko ya kikabila yamedumu miezi 8 sasa, na kusababisha vifo vya maelfu ya raia wa taifa hilo, na wengine kulazimika kuyahama makaazi yao na kukimbilia nje ya nchi.
Mkataba wa kusitisha mapigano umesainiwa na makundi hayo mwaili hasimu, pamoja na wawakilishi wa vyama vya kisiasa, wanadini, mashirika ya kiraia, na wajumbe wa mataifa ya kigeni waliohudhuria mkutano huo, akiwemo rais wa Congo Denis Sassou Nguesso.
Mkutano huo uliyowashirikisha wadau wote katika mzozo wa Jamhuri ya Afrika ya Kati kwa lengo la kuboresha maridhiano ya kitaifa na mazungumzo ya kisiasa, ulianza tangu jumatano, lakini baadhi ya malengo yake hayakufikiwa hususan suala la kupokonya silaha makundi yanayozimiliki kinyume cha sheria na mkataba wa muongozo kwa mchakato mzima wa kisiasa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati.
“Mkutano huo ni hatua ya mwanzo kabla ya mazungumzo ya kitaifa na mkutano kuhusu maridhiano ya kitaifa, ambavyo vitatamatisha mchakato mzima tuliyoanza na kujikubalisha mbele ya mataifa na raia wa Jamhuri ya Afrika ya Kati kwamba tutawumaliza”, amesema rais Sassou Nguesso.
Tangu kupinduliwa kwa utawala wa François Bozizé mwezi Machi mwaka 2003 na wapiganaji wa kundi la zamani la waasi la Seleka, ambao wengi wao ni kutoka jamii ya waislamu, taifa hilo liliingia katika machafuko ya kikabila.
Kwa sasa taifa hilo linakabiliwa na usalama mdogo, huku raia wengi wakiwa wameyahama makaazi yao wakihofia maisha yao, huku mamia kwa maelfu ya raia wakiwa wameuawa.