Burundi: kundi la waasi wa FNL lakiri kushambulia ngome za jeshi
Kundi moja la waasi nchini Burundi, limejigamba hapo jana kuhusika katika shambulio dhidi ya kituo kimoja cha kijeshi nchini humo karibu na mpaka na jamhuri ya kidemokrasia ya Congo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Waasi hao wamekiri kuwauwa wanajeshi sita katika shambulio hilo, idadi iliokanushwa na jeshi la taifa hilo.
Msemaji wa jeshi la Burundi kanali Gaspard Baratuza amefahamisha kwamba kulikuwa na makabiliano na kundi la wahuni, na kukanusha taarifa ya kupoteza wanajeshi, badala yake kuthibitisha kuwa wamemuua muasi mmoja katika shambulio hilo.
Kundi hilo la waasi linasadikiwa kuwa ni miongoni mwa wafuasi wa chama cha FNL walioasi na kuanzisha uasi. Kulingana na msemaji wa kundi hilo Felix Jean Ntahonguriye amethibitisha kwamba walishambulia kituo cha jeshi kilichopo katika tarafa ya Gihanga kwenye umbali wa kilometa zaidi ya Ishirini na jiji la Bujumbura na baadae kutokomea katika msitu wa Rukoko karibu na DRCongo.
Kundi hilo la waasi limekiri kuhusika na mashambulizi zaidi ya kumi liliyoendesha tangu mwanzoni mwa mwaka 2014,katika eneo hilo la Gihanga, likitokea mashariki mwa Jamhuri ya Congo. Kwa mujibu wa msemaji wa kundi hilo, wamepanga kuendesha mashambulizi dhidi ya ngome za jeshi hadi zitakapo fanyika chaguzi za mwaka 2015.
Msemaji wa jeshi, Gaspard baratuza, amepuuzia vitisho hivyo, akibaini kwamba kundi hilo halina nguvu yoyote, bali limekua waibia raia mali zao.
Burundi ni moja ya mataifa ya ukanda wa maziwa makuu yaliyokubwa na machafuku ya wenyewe kwa wenyewe ambayo yalidumu zaidi ya mwongo mmoja, na kusababisha vifo vya maelfu ya raia huku wengine wakilazimika kuyahama makaazi yao.