Chama tawala Burundi chainyooshea kidole cha lawama EU
Chama tawala nchini Burundi cha CNDD-FDD kimesema kuwa vikwazo vilivyowekwa na Umoja wa Ulaya dhidi ya baadhi ya viongozi wa serikali ya rais Pierre Nkurunziza ni "uchochezi" na vinalenga watu binafsi wa kabila la kihutu.
Imechapishwa:
Tamko hilo la chama tawala linasisitiza pia kuwa vikwazo hivyo vitadhoofisha mazungumzo yanayotarajiwa kufanyika na kuleta mgawanyiko kati ya Warundi kwa misingi ya kikabila na vinawalenga walioongoza mapambano ya mwaka 1993 hadi 2006.
Tarehe 1 Oktoba mwaka huu, Umoja wa Ulaya ulipiga marufuku kusafiri na kuwafungia akaunti za kifedha maafisa wanne amabo ni pamoja na Naibu mkurugenzi Mkuu wa Jeshi la Polisi Godefroid Bizimana, Mshauri wa rais katika masuala ya polisi Gervais Ndirakobuca (Ndakugarika), na afisa mwandamizi wa Usalama wa taifa Mathias Joseph Niyonzima (Kazungu) pamoja na aliyekuwa Naibu mkuu wa Idara ya ujasusi, jenerali Leonard Ngendakumana.
Viongozi hao wanadaiwa kutoa mchango wao katika ukandamizaji wa kikatili dhidi ya wapinzani wa awamu ya tatu ya Nkurunziza, kudhoofisha demokrasia au kushiriki katika "vitendo vya vurugu, ukandamizaji, na kuchochea ghasia katika mazingira ya mgogoro mkubwa ulioikabili Burundi tangu kutangazwa mwishoni mwa mwezi Aprili kwa mgombea urais Nkurunziza, wapinzani wake wakiamini kuwa ni kinyume na katiba.
Tayari Chama cha CNDD-FDD kiliwahi kushutumiwa kuanzisha tuhuma za uchochezi dhidi ya Watutsi kwa kusema kuwa ni wahusika wakubwa katika mgogoro wa kisiasa, jambo ambalo kwa maoni ya waangalizi, kimsingi ni la kisiasa na kuhofia nchi hiyo kurejea katika vurugu na mauaji baina ya makabila hayo mawili.