Rais mpya wa Namibia atawazwa, baada ya kifo cha rais Hage Geingob
Rais Mpya wa Namibia Nangolo Mbumba ametawazwa kuwa rais wa nne wa Namibia saa chache baada ya kifo cha rais Hage Geingob, aliyefariki hospitalini mapema siku ya Jumapili.
Imechapishwa:
Nangolo Mbumba ambaye alikuwa akihudumu kama makamu wa rais chini ya uongozi wa Geingob ametawazwa katika ikulu ya rais nchini humo.
Naye Netumbo Nandi-Ndaitwah ametawaza kuwa makamu wa rais mara moja.
Katika hotuba yake, Nangolo Mbumba amempongeza mtangulizi wake akimtaja kuwa mbunifu mkuu wa katiba na usanifu wa utawala wa Namibia.
Nangolo Mbumba ataongoza nchi kwenye uchaguzi utakaofanyika baada ya muda wa miezi 9.
Rais wa Namibia, Hage Geingob, aliyekuwa mtetezi wa uhuru na mpinzani mkubwa wa utawala wa kibaguzi, amefariki mapema Jumapili Februari 4 akiwa na umri wa miaka 82 hospitalini alikokuwa akitibiwa saratani, ofisi ya rais imetangaza.
Hage Geingob, aliyechaguliwa kuwa rais mwaka 2014, alifariki dunia mjini Windhoek, mji mkuu wa Namibia ambako alilazwa hospitalini baada ya kugunduliwa kwa seli za saratani wakati wa kufanyiwa uchunguzi wa kimatibabu, kulingana na ofisi ya rais.
Hage Geingob ambaye alichaguliwa kwa mara ya kwanza mnamo mwaka 2014, alichaguliwa tena mnamo mwaka 2019 kama rais wa Namibia, nchi ya jangwani inayopatikana kusini mwa Afrika, moja ya nchi za mwisho barani iliyepata uhuru mnamo mwaka 1990.