Waasi wa Huthi wapinga azimio la UNSC
Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa limepitisha azimio la kuwawekea vikwazo waasi wa Houthi kununua silaha na pia kuwataka kuondoka katika maeneo wanayoshikilia nchini Yemen ikiwa ni pamoja na jiji kuu Sanaa.
Imechapishwa:
Urusi haikupiga kura wakati wa kupitishwa kwa azimio hilo huku Marekani kupitia balozi wake Samantha Power akisema hatua zaidi zitachukuliwa kwa wale watakaoendelea kusababisha machafuko nchini humo.
Waasi hao wamelaani azimio hilo ambalo wanasema halikubaliki.
Kwa siku ya 21 ya operesheni ya vita vya dhidi waasi wa Huthi, muungano unoongozwa na Saudi arabia umeongeza mashambulizi dhidi ya ngome za waasi hao.
Jumatatu wiki hii, ndege za kivita za muungano huo, ziliendesha mashambulizi katika Ikulu ya rais Mansour Hadi inayoshikiliwa na wanamgambo wa kishia.
Wakati huohuo mapigano yanaendelea kurindima kwenye mpaka wa Saudi Arabia na Yemen.
Wachambuzi wa siasa za Kimataifa wanabaini kwamba mapigano yanayoendelea nchini Yemen yameendelea kuigawa nchi hiyo.