India:Wakuu wa mataifa ya G20 wakubaliana kuja na azimio la pamoja kuhusu Urusi
Nairobi – Mkutano wa siku mbili unaowaleta pamoja wakuu wa nchi kutoka mataifa yenye uchumi mkubwa duniani, za G20 umeanza jijini New Delhi, nchini India chini ya Mwenyekiti wa sasa Waziri Mkuu Narendra Modi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Viongozi hao wanajadili masuala mbalimbali kuhusu usalama wa chakula duniani, changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi lakini pia amani na usalama duniani, hasa vita vya Urusi nchini Ukraine.
Mataifa hayo yamekutana wakati huu kukiwa na mgawanyiko mkubwa kufuatia vita vya Ukraine na jinsi ya kuyasaidia mataifa yanayoinukia kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Mwenyekiti wa mkutano huo, Waziri Mkuu Modi, ametangaza kuwa wakuu wa nchi wamekubaliana kuja na azimio la pamoja kuhusu majadiliano yanayoendelea.
Katika siku ya kwanza ya mkutano huo, wakuu hao wamekubaliana umuhimu wa kuharakisha ufadhili wa fedha kukabili mabadiliko ya tabia nchi na kuyasaidia mataifa masikini.
Aidha, mataifa tajiri yametakiwa, kutekeleza ahadi yao ya kuchangia fedha na kuyasaidia mataifa masikini hasa barani Afrika yanayokabiliwa na athari ya mabadiliko ya tabia nchi na kusabisha kuongeza kwa kiwango cha joto, mafuriko na ukame.
Mkutano huo umebaini kuwa, vita vinavyoendelea nchini Ukraine vimesababisha mateso ya binadamu nchini humo, lakini Urusi haijashutumiwa moja kwa moja.
Kabla ya kuanza kwa mkutano huo, Umoja wa Afrika umekaribishwa kuwa mwanachama wa kudumu wa G 20. Mkutano huo hata hivyo haujahudhuriwa na marais wa Urusi, Vladimir Putin na Xi Jinping wa China.