Kundi la kwanza la waangalizi wa Umoja wa Mataifa UN lawasili nchini Syria
Kundi la kwanza la waangalizi wa Umoja wa Mataifa limewasili nchini Syria ikiwa ni hatua za mwanzo za kutekeleza maazimio ya baraza la usalama la Umoja wa mataifa la kupeleka waangalizi wake nchini humo.
Imechapishwa:
Kuwasili kwa waangalizi hao wa Umoja wa Mataifa ni miongoni mwa mapendekezo sita ya msuluhishi mkuu wa mgogoro huo Koffi Annan ambaye alitaka kuwepo kwa waangalizi hao watakaohakikisha kunakuwepo usitishwaji wa mapigano.
Msemaji wa UN Kieran Dwyer amethibitisha kuwasili kwa waangalizi sita wa umoja huo amba wataendelea kuandaa mazingira ya kuwasili kwa waangalizi zaidi wa umoja wa Mataifa.
Mpango huo pia ilikubaliwa na rais Bashar al-Assad ambaye alikubalina na mapendekezo ya Koffi Anna kama njia moja wapo ya kumaliza mzozo wa kisiasa unaoendelea nchini humo.
Licha ya kuripotiwa mashambulizi mapya yanayofanywa na vikosi vya Serikali, wizara ya mambo ya ndani nchini humo imedai kuwa mashambulizi yanayofanywa sasa ni kujibu mashambuli ambayo yanafanywa na baadhi ya vikundi ambayo vinashambulia vituo vya polisi.
Taarifa kutoka nchini humo zinasema kuwa waziri wa mambo ya nje wa Syria Walid Muallem amesafiri kuelekea nchini China ambako anatarajiwa kukutana na viongozi wa nchi hiyo kwenye mazungumzo yanayolenga kujadili mzozo unaoendelea nchini humo.
China imekuwa mshirika wa karibu wa rais Assad akiungwa mkono pia na nchi ya Urusi ambayo imetaka kutokuchukuliwa kwa hatua za uvamizi wa kijeshi dhidi ya Syria.