Marekani kutuma chombo maalum chini ya bahari kutafuta kisanduku cha ndege ya Malaysia
Wakati operesheni ya kusaka mabaki ya ndege ya Malaysia MH370 ikihamishiwa chini ya bahari, jeshi la Marekani limetuma chombo maalumu chini ya bahari chenye uwezo wa kubaini kisanduku cheusi cha mawasiliano.
Imechapishwa:
Kifaa hichi cha jeshi la Marekani chenye mitambo maalumu kina uwezo wa kubaini mahali kilipo kisanduku cheusi cha ndege ya Malaysia ambayo inadaiwa kuanguka kusini mwa bahari ya hindi kwenye bara la Australia.
Wataalamu wa masuala ya ndege wameonya kuwa zoezi hilo litakuwa gumu zaidi kwakuwa muda wa kisanduku cha mawasiliano kuwa na uwezo wa kukaa na umeme umekaribia kumalizika na hivyo itakuwa ngumu zaidi kukipata.
Kampuni ya Boeing iliyotengeneza ndege hiyo imesema kuwa kisanduku cheusi cha mawasiliano cha ndege zake kinauwezo wa kukaa kwa muda wa siku 30 na baada ya hapo hupoteza nguvu, hali ambayo ni wazi itaathiri zoezi la utafutaji wa ndege hiyo.
Hata hivyo wataalamu hao wamedai kuwa licha ya kuwa huenda kikapoteza uwezo wake, bado kunauwezekano wa kukipata iwapo mabaki ya ndege hiyo yatapatikana kama ilivyokuwa kwa ndege ya Air France iliyoanguka kwenye bahari ya Atlantic.
Ndege ya MH370 ya Malaysia ilipotea tarahe 8 ya mwezi uliopita ikielekea nchini China ikiwa na abiria wake 239 na mpaka sasa hakuna mabaki yoyote ya ndege hiyo yaliyobainika.