Afghanistan: Kiongozi Mkuu wa Taliban aamuru 'kutowaadhibu' maafisa wa zamani
Nchini Afghanistan, wakati mashirika mengi yasiyo ya kiserikali yakiutuhumu utawala wa Kiislamu kwa ghasia na mauaji ya kikatili, Mullah Hibatullah Akhundzada ametoa wito wa kuheshimiwa kwa msamaha wake katika hotuba adimu kwa maafisa wa Afghanistan huko Kandahar, kusini mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Kiongozi mkuu wa Taliban amezungumza baada ya video iliyosambazwa sana kwenye mitandao ya kijamii. Inafichua kisa cha kupigwa kwa afisa wa zamani wa jeshi katika jela na wapiganaji wawili wa Taliban.
Ripoti mbili za kusikitisha zilizochapishwa mwezi Desemba, moja kutoka Umoja wa Mataifa na nyingine kutoka shirika la kimataifa la Haki za Binadamu la Amnesty International, zilionyesha mamia ya mauaji ya kiholela yaliyotekelezwa na Taliban tangu kuchukuwa mamlaka dhidi ya watu wanaoshukiwa kufanya kazi katika serikali ya zamani.
Kiwango cha mauaji hakijulikani
Kulingana na Amnesty International, wapiganaji wa Taliban waliwaua kikatili raia kwa kuwapiga risasi kichwani, kifuani au moyoni. Mauaji ambayo ni "uhalifu wa kivita".
Mashahidi wanaripoti kwamba wakati baadhi ya watu waliouawa walihudumu katika vikosi vya ulinzi na usalama vya Afghanistan siku za nyuma, hakuna hata mmoja wao aliyekuwa akishiriki katika uhasama wakati walipouawa.