Shambulio la Iran nchini Israel limefanikiwa, yajigamba Tehran ikiionya tena Tel Aviv
Iran imefanya shambulizi kubwa dhidi ya Israel usiku wa Jumamosi Aprili 13 kuamkia Jumapili Aprili 14 kwa mamia ya ndege zisizo na rubani na makombora ya balestiki na ya usahihi wa hali ya juu, na kufikia hatua muhimu katika mzozo wa kikanda.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu mjini Tehran, Siavosh Ghazi
Huko Tehran, shambulio hilo linachukuliwa kuwa la mafanikio. Ni shambulio kubwa zaidi la ndege zisizo na rubani katika historia. Pia ni mara ya kwanza kwa Israel kupigwa hivi tangu vita vya mwaka 1967.
Wairani waliingia barabarani mjini Tehran na miji ya mikoa mbalimbali kutangaza ushindi na kueleza furaha yao.
Video nyingi pia zinasambaa kwenye mitandao ya kijamii zikionyesha makombora ya Iran juu ya msikiti wa Al-Aqsa mjini Jerusalem au juu ya Bunge la Israel (Knesset). Katika baadhi ya video, kunaonekana pia makombora yakilenga shabaha moja baada ya nyingine.
Onyo kwa Washington
Tehran imedai kwamba maeneo ya kijeshi yamelengwa, haswa kambi iliyoko Negev, lakini pia kambi ya kaskazini mwa Israeli ambayo ndege zilizopiga Aprili 1 zilitoka, na kuua watu kumi na sita, wakiwemo makamanda wawili muhimu wa Walinzi wa Mapinduzi.
Wakati wa usiku, Walinzi wa Mapinduzi walitoa taarifa ya kuionya Israel, lakini pia Marekani. Nakala inasema kwamba kama serikali ya Kiyahudi itaamua kujibu, wakati huo majibu ya Tehran yatakuwa makali zaidi.
Pia inaionya Marekani, ikisema kwamba iwapo Marekani itaungana na Israel kushambulia Iran, maslahi na misingi yote ya Marekani katika eneo hilo, hasa Syria na Iraq, yatalengwa bila kusita na mashambulio yatakuwa halali.