Lawrence Mulindwa ateuliwa kuwa naibu mwenyekiti wa CECAFA
Mwenyekiti wa shirikisho la soka Afrika Mashariki na Kati CECAFA Leodegar Tenga amemteua aliyekuwa rais wa shirikisho la soka nchini Uganda FUFA Lawrence Mulindwa kuwa Naibu wake. Tenga amesema kuwa Mulindwa ambaye alikuwa kiongozi wa FUFA kwa kipindi cha miaka minane ana uzoefu mkubwa katika maswala ya soka nchini Uganda na katika kamati ya CAF na atasaidia kuimarisha soka katika kanda ya CECAFA.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mbali na kuwa naibu mwenyekiti, Mulindwa pia alichaguliwa kuwa mmoja wa mwanakamati wa CEACAFA mwaka uliopita wakati wa uchaguzi wa shirikisho hilo jijini Nairobi nchini Kenya.
Katibu mkuu wa CECAFA Nicolas Musonye amesema kuwa uteuzi huo pia utasaidia kutafuta wafadhili wa kifedha kusaidia kufadhili michuano mbalimbali ya klabu bingwa na ile ya mataifa ya CECAFA ambayo hufanyika kila mwaka.
Mapema juma hili CECAFA ilivipongeza vlabu vya ukanda huo kwa kufuzu katika mzunguko wa pili wa michuano ya klabu bingwa barani Afrika na Shirikisho.
Baadhi ya vlabu vilivyofuzu katika hatua hiyo ni pamoja na Yanga FC ya Tanzania, Gor Mahia na AFC Leopards ya Kenya, KCC ya Uganda miongoni mwa wengine.