Urusi yashushia lawama mataifa ya magharibi
Rais wa Urusi Vladimir Putin ameendelea kusisitiza nchi yake kutohusika na machafuko yanayoendelea kushuhudiwa mashariki mwa Ukraine na kwamba vurugu hizo zimetokana na uchochezi unaofanywa na mataifa ya magharibi.
Imechapishwa:
Kwenye mazungumzo yake kwa njia ya simu na rais wa Marekani, Barack Obama ambaye ameituhumu Urusi kwa kuwa chanzo cha machafuko nchini humo, rais Putin alimjibu kwa kudai kuwa nchi yake haiusiki na itaendelea kuwalinda raia wake walioko nchini Ukraine.
Telephone conversation with Barack Obama: discussion of joint diplomatic efforts to resolve the crisis in Ukraine http://t.co/gn9tv0JSbW
— President of Russia (@KremlinRussia_E) April 15, 2014
Katika hatua nyingine viongozi wa Umoja wa Ulaya EU wamekutana mjini Brussels Ubelgiji na kuzungumzia kuhusu mzozo wa Ukraine ambapo wameitaka Urusi kutoingilia masuala ya nchi hiyo ambapo wameitisha vikwazo zaidi dhidi ya Urusi.
Mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya, Catherine Ashton, amesema watawaweka vikwazo vya usafiri na fedha dhidi ya viongozi wa Urusi.
Wakati huohuo katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon kupitia kwa msemaji wake, Stephane Dujarric amesema kuwa ni kwa njia ya mazungumzo pekee tena ya uwazi ambayo yanaweza kumaliza mzozo wa Ukraine.
Mzozo wa Ukraine umeendelea kuwa mgumu zaidi licha ya rais wa mpito, Oleksandr Tuchinov kuomba msaada wa Umoja wa Mataifa kukabiliana na makundi ya watu wenye silaha wanaoendelea kuteka vituo vya polisi na ofisi za Serikali kwenye miji ya mashariki mwa nchi hiyo.