DRC : mji wa Kisangani wapokea waasi wa FDLR
Waasi wa kihutu wa Rwanda FDLR wamekusanywa kwa makubaliano na serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo katika mji wa Kisangani, baada ya waasi hao kukubali kuweka silaha chini na kuwa tayari kuketi kwenye meza ya mazungumzo na serikali ya Kigali, japo kuwa serikali hio imefutilia mbali kuketi kwenye meza moja na waasi hao.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa msemaji wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Charles-Antoine Bambara, wapiganaji 570 wa FDLR pamoja na familia zao ndio watakao kuwa wa kwanza kupiga kambi katika mkoa wa Oriental Kaskazini-Mashariki mwa nchi hiyo.
Aidha, Bambara amebainisha kuwa waasi wa FDLR watabaki katika eneo hilo la Kisangani hadi itakapotajwa nchi nyingine ambayo itakuwa tayari kuwapokea na kuwapa hifadhi.
Kambi moja ya zamani ya kijeshi imekarabatiwa kwa ajili ya kuwapa hifadhi waasi hao, hatua ambayo inapingwa na kukosolewa na baadhi ya taasisi zisizo za kiserikali na za kutetea haki za binadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Itakumbukwa kuwa mji huo umeshuhudia mapigano makali baina ya jeshi la aliekua rais Mobutu na waasi wa zamani wa Laurent Desire-Kabila, na baadaye mapigano ya siku sita baina ya askari wa Rwanda na wa Uganda.