Kenya: William Ruto aapishwa kama rais
William Ruto ameapishwa Jumanne Septema 13, 2022 kuwa rasmi rais wa tano wa Jamhuri ya Kenya, baada ya uchaguzi mkali lakini wa amani. Sherehe zimefanyika katika uwanja wa Moi Kasarani katika sherehe iliosimamiwa na msajili wa idara ya mahakama Anne Amadi na kushuhudiwa na jaji mkuu Martha Koome.
Imechapishwa:
Hafla ya kuapishwa kwa Ruto imehudhuriwa na viongozi mbalimbali duniani akiwemo Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Yoweri Museveni wa Uganda, Paul Kagame wa Rwanda, Evariste Ndayishimiye wa Burundi, Felix Tshisekedi wa Jamhuri ya Demokrasia ya Congo, Salva Kiir wa Sudan Kusini, Emmerson Mnangagwa wa Zimbabwe, Nana Akufo-Addo wa Ghana, Lazarus Chikwera wa Malawi na Waziri Mkuu Ethiopia Abiy Ahmed.
"Mimi, William Samoei Ruto (...) naapa kuihifadhi, kuilinda na kuitetea Katiba ya Kenya (...) kama Rais", alitangaza Mkuu huyo mpya wa Nchi, akila kiapo cha Katiba na kushikilia Biblia moja mkononi, katika uwanja wa Moi Kasarani, katika mji mkuu wa Nairobi.
Baadaye bendera na picha ya rais anayeondoka mamlakani ilishushwa huku bendera na picha ya rais mpya ikipandishwa, kabla ya mizinga ishirini na moja kupigwa ikiashiria utawala mpya.
Ruto amekula kiapo cha kuwa rais wa tano wa Kenya na kumrithi Rais Uhuru Kenyatta aliyemaliza mihula miwili ya miaka mitano kila mmoja.
Mapema leo, watu kadhaa walijeruhiwa wakati umati wa watu ulijaribu kuingia kwa nguvu uwanjani hapo huku picha za televisheni zikionyesha watu kadhaa wakiangukiana na kukanyagana katika mojawapo ya malango.