Kenya: Rais Ruto amemshutumu mtangulizi wake kwa kuunga mkono maandamano
Nairobi – Nchini Kenya, rais William Ruto sasa amemwonya mtangulizi wake Uhuru Kenyatta kwa madai ya kuendelea kushirikiana na kinara wa upinzani Raila Odinga.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Rais Ruto, akizungumza katika mji wa Mai Mahiu kaunti ya Nakuru, kwenye mkoa wa bonde la ufa siku ya Ijumaa, alidai kuwa Uhuru amekuwa akifadhili kwa siri maandamano ya Odinga dhidi ya serikali ambayo hivi majuzi yaligeuka kuwa vurugu huku vifo vingi vikiwa vimerekodiwa.
'Tutakusafirisha na yeye,' President Ruto now warns Uhuru over association with Raila pic.twitter.com/fVZpD7EPhp
— NTV Kenya (@ntvkenya) July 14, 2023
Haya yanajiri wakati huu rais Ruto akimtahadharisha Odinga dhidi ya kuendelea na maandamano yake yaliyopangwa kufanyika kwa siku tatu wiki ijayo, akisema kwamba serikali itamchukulia hatua kali iwapo atafanya hivyo.
Rais alionya kwamba, ingawa kufanya maandamano ni haki ya raia yeyote kama ilivyoainishwa katika Katiba, Odinga atakabiliwa vikali na vyombo vya usalama iwapo umwagaji damu zaidi utashuhudiwa katika mchakato huo.
Ruto aliapa kumkabili kikamilifu Odinga kisiasa na kuhakikisha kwamba anastaafu na kurejea nyumbani kwake Bondo Magharibi ya Kenya.
Mkuu wa nchi aliongeza kuwa iwapo rais wa zamani Kenyatta ataendelea kufadhili maandamano ya Odinga, basi huenda pia atalazimishwa kusataafu na rafiki yake Odinga.
“Nataka nimwambie rafiki yangu Uhuru, ata wewe wachana na huyu mzee (Odinga), wacha kumpatia pesa ya kununua watu wa Mungiki ( kundi ambalo limeharamishwa na serikali) wachome Nairobi. Wewe umekuwa rais, kuwa mungwana, tulikuunga mkono ulikuwa rais wetu, uliunga mtu wa kitendawili mkono tukamwangusha, wachana na yeye,” alisema.
Rais Ruto kuhusu wanaofadhili maandamano
“Usipowachana na yeye, ata wewe tutakusafirisha na huyo kitendawili wako. Uhuru Kenyatta tulimsaidia akiwa Rais, sasa kupanga Nairobi, imemkosea nini?”
Aidha rais alisisitiza kwamba Odinga ndiye aliyesababisha serikali iliyopita, chini ya Uhuru Kenyatta, kushindwa kutimiza ahadi zake kikamilifu, hivyo hatamruhusu kufika popote karibu na utawala wa Kenya Kwanza.