ICJ kutoa uamuzi katika kesi ya 'mauaji ya halaiki' dhidi ya Israel katika Ukanda wa Gaza
Mahakama ya juu zaidi ya Umoja wa Mataifa imetangaza siku ya Jumatano kwamba itatoa uamuzi wake siku ya Ijumaa kuhusu hatua za haraka zilizoombwa na Afrika Kusini, ambayo inaishutumu Israel kwa "mauaji ya kimbari" ya Wapalestina katika Ukanda wa Gaza.
Imechapishwa:
Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ), iliyoko Hague, inaweza kuagiza Israeli kusitisha kampeni yake ya kijeshi huko Gaza, iliyochochewa na shambulio la Hamas mnamo Oktoba 7, 2023.
Majaji 15 katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) wanachunguza kesi ya Afrika Kusini dhidi ya Israel kuhusu mashtaka ya kufanya mauaji ya kimbari dhidi ya raia wa Palestina wakati wa vita huko Gaza.
Afrika Kusini inataka ICJ kuilazimisha Israel kusitisha operesheni zake za kijeshi huko Gaza, ambapo inasema Israel inafanya mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina, na ICJ iyazingatie matendo ya Israel kwenye ardhi hiyo ya Wapalestina chini ya Mkataba wa Kimataifa wa kuzuia mauaji ya kimbari uliopitishwa mwaka 1948.
PRESS RELEASE: the #ICJ will deliver its Order on the request for the indication of provisional measures submitted by South Africa in the case #SouthAfrica v. #Israel this Friday, 26 January 2024, at 1 p.m. (The Hague). Watch live on @UNWebTV https://t.co/tikn2TSa8U pic.twitter.com/2csTaDZVZ1
— CIJ_ICJ (@CIJ_ICJ) January 24, 2024
Kulingana na mkataba huo, mauaji ya kimbari ni matendo yanayosababisha vifo vya watu wengi kwa lengo la kusambaratisha kwa sehemu au kwa jumla, taifa zima, kabila au jamiii ya watu wa rangi ama dini moja. Afrika Kusini na Israel zote zimesaini mkataba huo ambao unazilazimisha kutofanya mauaji ya kimbari na pia kuyazuia na kuyaadhibu.
Shambulizi la Hamas halihalalishi uvunjaji wa mkataba wa mauaji ya kimbari
Akizungumza katika ufunguzi wa kesi hiyo, Wakili wa Mahakama Kuu ya Afrika Kusini, Adela Hassim alisema shambulizi la Oktoba 7 la Hamas, haliwezi kuhalalisha Israel kuvunja Mkataba wa Mauaji ya Kimbari.
Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa alisema hatua yao ya kupinga mauaji ya watu wa Gaza, iliwasukuma wao kama nchi kufungua kesi ICJ.
Hata hivyo, Israel ilikanusha shutuma za kufanya mauaji ya kimbari, ikisema hazina msingi wowote na ilisema kuwa inafanya kazi kwa mujibu wa sheria za kimataifa.