Pata taarifa kuu
AFCON 2019-MISRI-AFRIKA KUSINI-IVORY COAST

Ivory Coast na Afrika Kusini, nani ataanza vizuri ?

Michuano ya soka kuwania taji la mataifa ya Afrika, inaingia katika wiki ya pili siku ya Jumatatu nchini Misiri, huku mechi tatu zikitarajiwa kuchezwa.

Wachezaji wa Tunisia wakifanya mazoezi
Wachezaji wa Tunisia wakifanya mazoezi cafonline.com
Matangazo ya kibiashara

Ivory Coast, mabingwa wa mwaka 2015, watakuwa wa kwanza kuingia uwanjani dhidi ya Afrika Kusini, katika mechi ya kundi D.

Mechi hii itachezwa katika uwanja wa Al Salam, jijini Cairo.

Kuelekea katika mechi hii, kocha Ibrahima Kamars anaamini kuwa kikosi chake kimejiandaa vizuri kupata alama tatu muhimu, na wachezaji chipukizi kama Nicolas Pepe, watatikisa nyavu za Afrika Kusini.

Timu hizi mbili zinakutana miaka 21, mara ya mwisho, zilipokutana katika michuano hii, ilipofanyika nchini Burkina Faso na matokeo kuwa sare ya 1-1.

Naye kocha wa Afrika Kusini, Stuart Baxter, amesema wachezaji wake wanakwenda katika michuano hii wakiwa na lengo la kupata alama zote tatu, katika mechi hii ya kwanza.

Kocha Baxter anamtegemea mchezaji Percy Tau mshambuliaji mwenye umri wa miaka 25 kufufua matumaini ya Bafana Bafana kushinda taji hilo ambalo walishinda mara ya mwisho mwaka 1996.

Morocco ilianza vema, baada ya kupata ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Namibia.

Mchezaji wa Namibia Itamunua Keimuine alijifunga na kuipa zawadi ya bao, Morocco katika ya 89 katika mchuano huo ambao ulikuwa mgumu katika uwanja wa Al Salam, jijini Cairo mwishoni mwa wiki iliyopita.

Mechi za kundi E, pia zinachezwa siku ya Jumatatu.

Angola v Tunisia

Mechi hii itachezwa saa mbili usiku saa za Afrika Mashariki katika uwanja wa Suez, mjini Suez.

Timu hizi zimekutana tu mara mbili katika historia ya michuano hii, na mara ya mwisho ilikuwa ni miaka 11 iliyopita nchini Ghana, ilipotoka sare ya kutofungana, matokeo ambayo yaliwasaidia kufika katika hatua ya robo fainali.

Kocha wa Tunisia Alain Giresse amesema lengo ya timu yake ni kufika katika hatua ya robo fainali ya michuano hii, licha ya kufahamu upinzani mkali.

Mali v Mauritania- Mechi hii itachezwa kuanzia saa tano usiku.

Mali inaanza mechi ya ufunguzi, baada ya maafisa wa soka nchini humo kutishiwa.

Aidha, kocha wa Mohamed Magassouba alichelewa kukitaja kikosi cha wachezaji wake wa mwisho kuelekea katika michuano hii.

Mauritania wamefuzu katika michuano hii kwa mara ya kwanza, na kocha Corentin Martins, raia kutoka Ufaransa anasema wachezaji wapo nchini Misri kushindana na kushinda mechi kadhaa.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.