Marekani yaitaka Urusi kuacha kuwasaidia wapiganaji wa Ukraine
Rais wa Marekani Barrack Obama ametoa wito kwa rais wa Urusi Vladimir Putin kuacha kusafirisha silaha nchini Ukraine pamoja na kuacha kuwaunga mkono wapiganaji wanaounga mkono serikali yake.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Ikulu ya Marekani inasema rais Obama amempigia simu rais Putin na hata kumtishia kuwa ikiwa haitasitisha kuingilia maswala ya Ukraine itaiwekea vikwazo zaidi.
Urusi imeendela kukanusha kuwaunga mkono wapiganaji Mashariki mwa Ukraine na kuwahami kwa silaha.
Ikulu ya Urusi inasema rais Putin kwa upande wake amekuwa akijitahidi sana kushinikiza mazungumzo ya amani kati ya wapiganaji hao na serikali ya Kiev.
Wapiganaji wanasema kwa sasa wanatii usitishwaji wa mapambano uliotangazwa na rais Petro Poroshenko kabla ya kukamilika siku ya Ijumaa juma hili.
Siku ya Jumatatu, Msemaji wa Ikulu ya Marekani Josh Earnest alisema rais Obama alizungumza na rais Putin na kumwomba kuchagua njia ya amani badala ya kuendelea kuwaunga mkono wapiganaji Mashariki mwa Ukraine.
Marekani na Umoja wa Ulaya tayari zimeiwekea vikwazo serikali ya Urusi, ikiwa vikwazo vya kutosafiri barani Ulaya na Marekani viongozi wa juu wa serikali ya Urusi pamoja na kuzuia mali zao.
Mataifa ya Magharibi, yanaendelea kuishinikiza serikali ya Ukraine kuzungumza na viongozi wakuu wa wapiganaji hao waliokubali kuacha mapigano ili kupatikana kwa suluhu la kudumu.
Rais Poroshenko amesisitiza kuwa ataweza tu kuzungumza na wapiganaji hao ikiwa watasitisha mapigano ambayo yamesabisha vifo Mashariki mwa nchi hiyo.
Porishernko pia ameendelea kuwashinikiza viongozi wa dunia kuhakikisha kuwa Urusi haiwaungi mkono wapiganaji hao na kusitisha kuwapa silaha.