Bei ya mafuta yaongezeka kufuatia mashambulizi ya Urusi didi ya Ukraine
Bei ya mafuta imeongezeka kwa zaidi ya dola tano kwa pipa, huku masoko ya hisa yakianguka, baada ya Rais wa Urusi Vladimir Putin kutangaza kuanzisha mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Ukraine.
Imechapishwa:
Masoko ya hisa yameanguka kwa asilimia 4 huku wafanyabiashara wakitathmini namna mataifa ya Magharibi yatajibu uvamizi wa Putin.
Bei ya mafuta ghafi imepanda na kufikia dola 100 kwa pipa mjini London, ikiwa ni mara ya kwanza tangu mwaka 2014, kutokana na wasiwasi kwamba huenda usafirishaji wa bidhaa hiyo kutoka Russia ukaathirika. Russia ni ya tatu katika uzalishaji wa mafuta duniani.
Hisa katika soko la Wall Street zimeshuka kwa asilimia 2.5.
Mashambulizi hayo yamechochea Washington na Ulaya kuapa kuiwekea Moscow vikwazo vikali, ambavyo huenda vikaathiri uchumi wa dunia.
Kwa upande mwengine rais wa tume ya Umoja wa ulaya Ursula Von der Leyen amesema kwamba mataifa 27 ya umoja huo yamepanga kutangaza vikwazo vikali dhidi ya Russia, na kwamba rais atawajibishwa ipasavyo.