EU yahamasisha kupambana dhidi ya Ebola
Mataifa ya Magharibi yameanza kuchukua tahadhari katika viwanja vya ndege na mipaka yao kutokana na kuendelea kusambaa kwa ugonjwa hatari wa Ebola.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Rais wa Marekani Barrack Obama tayari amesema nchi yake inaweka mikakati kuzuia Ebola kusambaa baada ya muuguzi wa pili kuambikizwa katika jimbo la Texas.
Mbali na Marekani, Ufaransa, Uingereza na Uhispania ni baadhi ya mataifa ambayo yamechukua tahadhari hiyo hasa kwa abiria wanaoingia nchini mwao kutoka Liberia,Guinea na Siera Leone kulikoathiriwa zaidi na ugonjwa huo.
Shirika la afya duniani limesema zaidi ya watu elfu nne wamepoteza maisha nchini Liberia, Siera Leone na Guinea.
Idadi ya wagonjwa wa Ebola inaendelea kuongezeka katika mataifa yanaoathiriwa ya Afrika Magharibi. Hayo yanajiri wakati mawaziri wa afya kutoka mataifa ya Ulaya wamekutana Alhamisi wiki hii Oktoba 16 mwaka 2014 mjini Brussels ili kutahmini mpango wa pamoja wa kupambana na homa hiyo ya Ebola.
Virusi vya Ebola vinasambaa kwa haraka. Kati ya wiki tatu na nne ziliyopita, idadi ya watu waliyokua wanaambukizwa virusi vya Ebola kwa wiki ilikua 600, kwa sasa watu 1000 wanaambukizwa virusi hivyo kwa wiki, kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani WHO.
Kulingana na utabiri wa shirika hilo, watu 10,000 watakua wakiambukizwa virusi hivyo kwa wiki ifikapo mwezi Desemba, iwapo hatua za kudhibiti Homa hiyo hazitachukuliwa haraka iwezekanavyo.