Burundi: Mwanahabari Sandra Muhoza anazuiliwa na idara ya ujasusi
Maafisa wa ujasusi nchini Burundi, wanamshikilia mwanahabari Sandra Muhoza, aliyetoweka siku ya Jumamosi baada ya kwenda kumhoji mfanyabiashara maarufu, aliyekaribu na chama tawala CNDD FDD, lakini hakuonekana tena.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Cheza - 00:56
Familia ya Mwanahabari huyo, mama wa watoto watatu, imethibitisha kushikiliwa kwa mpendwa wao, anayefanya kazi na jarida la mtandaoni, La Nova Burundi.
Ripoti zaidi zinasema alikamatwa siku ya Jumapili na anazuiwa kwenye jiji la kibiashara la Bujumbura.
Pascal Ndayisenga , Mkurugenzi wa La Nova Burundi amesema wana wasiwasi kuhusu kukamatwa kwa wenzao na mpaka sasa hijafahamika ni kwa nini anazuiwa.
Shirika la Kimataifa ka kutetea haki za wanahabari RSF nalo limelaani kukamatwa kwa Sandra na kutaka kuachiwa kwake.
Serikali ya rais Evariste Ndayishimiye, aliyeingia madarakani mwaka 2020, imekuwa ikishtumiwa kwa kushindwa kuimarisha haki za binadamu nchini humo, huku uhuru wa wanahabari ukiendelea kushuka na kuwafanya kuishi kwa woga.
Soma piaE. Ndayishimiye: 'Hatuna hofu ya chochote kuhusiana na haki za Binadamu nchini Burundi'
Jumapili iliyopita, Maaskofu wa Kanisa Katoliki, walitoa taarifa ya kushtulu hali ya kisiasa na usalama nchini Burundi, wakilaani kukamatwa na kupotezwa kwa wapinzani na serikali na kuonya kuwa nchi hiyo ipo kwenye hatari ya kurejea kwenye utawala wa chama kimoja.