Kenya mbioni kukuza ushirikiano na ICC
Serikali ya Kenya inasema hivi karibuni itafungua kitengo maalum katika Mahakama Kuu kushughulikia kesi kuhusu makosa yanayogusa sheria za Kimataifa.
Imechapishwa:
Kauli hii imetolewa na Mwanasheria Mkuu Githu Muigai jijini Nairobi ambaye amesema pia kuwa, serikali itawasiliana na Mahakama ya Kimataifa ya ICC ili kukabidhiwa majalada matatu ya Wakenya wanaotafutwa na Ofisi ya kiongozi wa Mashtaka kwa tuhma za kuwahonga na kuwatisha mashahidi waliokuwa wanapanga kutoa ushahidi dhidi ya washukiwa waliokuwa katika Mahakama ya ICC kujibu mashtaka ya kufadhili na kuchochea machafuko ya baada ya uchaguzi Mkuu mwaka 2007.
Haya yanajiri siku chache tu baada ya Majaji wa Mahakama ya ICC kufuta mashtaka dhidi ya Makamu wa rais William Ruto na Mwanahabari Joshua Arap Sang.
Katika hatua nyingine, Kenya inasema haitajiondoa kama nchi mwanachama wa kanuni za Roma zilizounda Mahakama hiyo lakini wakati ukifika itajiondoa kwa pamoja na mataifa mengine ya bara la Afrika.